Pages

Thursday, November 14, 2013

HAWA GHASIA AGEUKA MBOGO WILAYANI CHUNYA




Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) juzi aligeuka mbogo na kutaa kupokea taarifa ya maendeleo iliyotolewana na Kaimu MKurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Chunya, Mbeya, Charles Mwakalila, baada ya kubainika kufichwa kwa mambo muhimu hususani takwimu sahihi za Fedha za miradi elimu, barabara na Maji.

Waziri Ghasia aligomea taarifa hiyo juzi mbele ya watumishi wa idara mbalimbali wa halmashauri hiyo wakati wa kikao baina yake na watumishi aliowakutanisha kwa lengo la kuwasikiliza kero zao na kuzijibia.

Aidha, Waziri Ghasia, alianza kubaini madudu  hayo mwanzoni kabisa mwa ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo ukiwemo wa mradi wa ujenzi wa chumba cha Maabara kwa Shule ya Sekondari ya Chokaa ambapo alionesha wasiwasi wake baada Kaimu Mkurugenzi, Mhandisi  wa majengo wilaya Mkombozi Cyrille na Ofisa mipango wilaya, Erasto Mbilinyi, kutaja viwango vya fedha vinavyotofautiana ya ujenzi wa chumba hicho.

“Jamani siwezi kuweka jiwe la msingi kwenye mradi huu wenye ubabaishaji kwani nauliza benki ya dunia imelewatea kiasi gani Mkurugenzi anasema Sh270 milioni, mhandisi anasema 176 haya Ofisa mipango hapa naye ana jibu lake na hamjui kama mimi najua fika fedha zilizoletwa hapa halafu mnanidanganya,” alisema Waziri.

Hata hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro alimuomba radhi kwa mkanganyiko huo na kumsihi  kuweka jiwe hilo jambo ambalo Waziri alifungua jiwe hilo kwa shingo upande tena kwa kutumia mkono mmoja wa kushoto huku akitazama pembeni badala ta kusoma maandishi yaliyokuwa yameandikwa kwenye jiwe hilo.

Hata hivyo hali ikawa tete zaidi ndani ya kikao na watumishi baada ya  kusomewa taarifa ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ambapo alisema kuwa hawezi kupokea taarifa iliyojaa taarifa za kizushi huku akibainisha wazi mambo ya msingi ambayo yanatakiwa yawekwe wazi kwa wananchi yamefichwa

“Hapa haiwezekani hawa wakuu wa idara lazima kuna kitu mheshimiwa Mkuu wa Mkoa kwanini wanaficha takwimu sahihi na muhimu za fedha za umma na kila mkuu wa idara nikimuuliza fedha za mradi fulani ziko wapi anashindwa kuzisemea na Mkurugenzi wenyewe anaongopa hata kiasi cha fedha alizosaini mbele yangu za miradi ya maji, nasema hivi hii taarifa sipokei,”alisisitiza Waziri Ghasia.

Alisema kuwa katika ziara yake alitegemea kupewa taarifa za miradi iliyotengewa bajeti kwa kuzingatia vipaumbele  vilivyopo kwenye Mpango wa matokeo makubwa sasa (BRN) lakini imekuwa kinyume chake huku kukiwa na majibu sahihi juu ya fedha hizo zimekwenda wapi.

Aidha,  Waziri alisema kuwa miongoni mwa miradi ambayo fedha yake wakurugenzi walishasainishwa ni pamoja na fedha za miradi ya maji, barabara na elimu lakini matokeo yake hakuna hata kimoja kati ya hivyo vinavyooneshwa kama utekelezaji wake umefikia wapi.

Baada ya  mkanganyiko huo Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro aliposimama alisema kuwa hata yeye anashindwa kuelewa mdudu aliyewachanganya watumishi hadi hadi kufikia kujikanyaga kanyaga ovyo ovyo mbele yake.

  Na  Godfrey Kahango,Chunya

0 comments: