Pages

Monday, March 28, 2016

WAJAWAZITO WALALAMIKIA KUTOLEWA LUGHA CHAFU NA WATOA HUDUMA

 WAJAWAZITO. wa kata ya Igale wilayani Mbeya mkoani hapa wamelalamikia  kufukuzwa na kunyimwa huduma za uzazi kutoka kwa baadhi ya watoa huduma katika  zahanati za vijiji kwa madai  ya kuwa wananuka.



Hayo yameelezwa juzi wakati wa mrejesho wa yaliyojiri kwenye utafiti wa siku tano uliofanywa na maofisa wa Mtandao wa Jinsia wa TGNP kwenye kata ya Igale wilayani Mbeya juu ya tatizo la huduma za kijamii zinazotolewa kwa wakazi wa vijiji vitano vya Horongo, Izumbwe, Shongo na Igale.



Akizungumza katika kikao kilichowahusisha wanahabari wa vyombo mbalimbali mkoani Mbeya, Naye Mwenyekiti wa Kituo cha Taarifa na Maarifa TGNP kata ya Igale Lyidia Sankemwa alisema kuwa akina mama wajawazito wamekuwa wakifukuzwa kwenye zahanati wakidaiwa kuwa ni wachafu wananuka.



‘’Tumepokea malalamiko mengi kutoka kwa wakina mama wajawazito kuwa  baadhi ya watoa huduma za afya  katika zahanati zetu  huwafukuza akina mama wajawazito,  kwa madai kuwa  wananuka na hatinaye kucheweleshewa  kupatiwa huduma,’’alisema 



Alifafanua kuwa tatizo hilo limekuwa kubwa maeneo ya vijijini kutokana na kukosekana huduma za uzazi kwa akina mama na mtoto na kuwa katika baadhi ya maeneo akina mama husafiri zaidi ya kilomita 10 kufuata huduma ya wazazi.



Naye katibu  wa kituo hicho, Alfred Mwambugu alisema kuwa kutokana na tatizo hilo baadhi ya  akina mama wamekuwa wakikata tamaa ya kwenda kupata huduma katika zahanati hizo kwa kuhofia kutolewa lugha chafu  na hivyo kujifungulia nyumbani hali ambayo ni hatari kwa maisha yao.



Akizungumzia malalamiko hayo Ofisa habari wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya Hamza Mwangomale alisema  ameyapokea malalamiko hayo na kwamba  tayari ameshawasiliana na mratibu wa afya kwa ajili ya kwenda kufanya kikao cha pamoja na watoa huduma za afya katika zahanati hizo.



“Hili suala ninauwezo nalo nitalishughulikia mara moja ili kuhakikisha malalamiko hayo yanafanyiwa kazi tunaandaa utaratibu wa kukutana na watoa huduma za afya katika kata hiyo ya igale ili kuweza kulizungumza  kwa pamoja na kuchukua hatua kwa wale watakaobainika wanatabia hizo”alisema



Kwa upande wake Ofisa Mtendaji wa Kata ya Igale Alinanuswe Mwakamala , alisema kata hiyo yenye jumla ya vijiji vitano ina  zahanati nne ambazo hazitoshelezi kwa kuhudumia wakazi wote wa kata hiyo hali ambayo inasababisha baadhi ya akina mama kuchelewa kupatiwa huduma hiyo kwa wakati.



Alisema  kata hiyo ina jumla ya wakazi 11,800 ambao hupata huduma kwenye zahanati nne na kuwa kijiji kimoja cha Horongo hakina zahanati hivyo wakazi wake hulazimika kufuata huduma hiyo kwenye zahanati za vijiji vingine umbali wa kilomita tano.


Na Brandy Nelson

0 comments: